Tuesday, 20 September 2016

TAFAKARI YA MASOMO YA MISA, 20/9/2016 Juma la 25 la Mwaka.


TAFAKARI
Jumanne, Septemba 20, 2016.
  Juma la 25 la Mwaka
Kumbukumbu ya Watakatifu Andrea Kim Taegon na Wenzake Mashahidi
       Mit 21: 1-6,10-13 Zab 118: 1, 27, 30, 34-35, 44 Lk 8: 19-21

    FAMILIA YA MUNGU!
         Familia changa kwa kawaida inaonekana kuwa na umoja na mshikamono zaidi kwa mtazamo wa hapa duniani. Lakini, Yesu anatufundisha kwamba kuna uhusiano na umoja wa karibu zaidi kuliko wa familia, umoja na mshikamano alio nao kati yake na wafuasi wake. Hili ndilo fundisho tunalo pata kutoka katika Injili ya leo. Yesu alikuwa amesimama mbele ya umati wa watu akiwafundisha na mara moja ukaja ujumbe, kwamba Mama yake na ndugu zake walikuwa wakisimama nje wakitaka kumuona. Jibu lake kwao linaonekana kama anamkataa Mama yake. Haikatai familia yake na wala hakuonesha kwamba haina umuhimu, na wala hakufundisha kwamba familia ya Kibinadamu ina nafasi ndogo kwa Mungu. Yeye anatangaza kuhusu uwepo wa familia ya pekee-familia ya kiroho. Familia ya kiroho na uhusiano wake umejikita katika Neno la Mungu-kulisikia na kuliishi. Mtu aliye karibu na Mungu ni mtu anaye mtii Mungu, anaye chukulia neno lake kwa umakini. Yesu anasema wale wanao lishika neno lake na kuliishi ndio Mama, Kaka na ndugu zake. Bikira Maria Mama yake, ndiye wakwanza kabisa kulisikia neno la Mungu na kulitenda katika ukamilifu wote, kwa hiyo unaweza kuona kwamba Yesu hakumkataa Mama yake bali alitaka sisi nasi tuwe ndugu zake kwa kuishi katika kulishika neno lake. Sisi tutakuwa ndugu wa Yesu kweli kama tutaishi kadiri ya Mafundisho yake. Tunaweza kusema tunampenda Yesu kweli kama tunashika yale aliyo tufundisha. Tusizibe masikio yetu kwa wenzetu wala kwa maskini wanapo kuwa na shida kwasababu sisi tunakuwa familia moja na Yesu na wala tusitamani uovu kwasababu kiongozi wetu hana uovu ndani yake. Sala: Bwana, tufanye ndugu zako kamili na wa kweli tukiwa tumejiunga katika familia kubwa ya kiroho. Amina

Copy right© by shajara and published by MAMBO YAHUSUYO IMANI BLOG 
website:


MASOMO YA MISA, 20/9/2016 Jumanne ya 25 ya Mwaka- C


KUMBUKUMBU YA WAT. ANDREA KIM TAEGON NA WENZAKE MASHAHIDI

SOMO LA 1
Mit. 21:1 – 6, 10 – 13
          Moyo wa mfalme huwa katika mkono wa Bwana; kama mfereji wa maji huugeuza popote apendapo. Kila njia ya mtu ni sawa machoni pake mwenyewe; bali Bwana huipima mioyo. Kutenda haki na hukumu humpendeza Bwana kuliko kutoa sadaka. Macho yenye kiburi, na moyo wa kutakabari, hata ukulima wa waovu, ni dhambi. Mawazo ya wenye bidii huuelekea utajiri tu; bali kila mwenye pupa huuelekea uhitaji. Kupata akiba ya mali kwa ulimi wa uongo ni moshi upeperushwao; ni kutafuta mauti. Nafsi ya mtu mbaya hutamani maovu; jirani yake hapati fadhili machoni pake. Mwenye mzaha aadhibiwapo, mjinga hupata hekima; na mwenye hekima afundishwapo, hupokea maarifa. Mwenye haki huitafakari nyumba ya mtu mbaya; jinsi wabaya waangushwavyo wakaangamia. Azibaye masikio yake asisikie kilio cha maskini, yeye naye atalia, lakini hatasikiwa. 

      WIMBO WA KATIKATI
     Zab. 119:1, 27, 30, 34 – 35, 44
        (1).  Heri walio kamili njia zao, Waendao katika sheria ya Bwana. Unifahamishe njia ya mausia yako, Nami nitayatafakari maajabu yako.
            (K) Uniendeshe katika mapito ya maagizo yako, Ee Bwana.
       (2).   Nimeichagua njia ya uaminifu, Na kuziweka hukumu zako mbele yangu. Unifahamishe nami nitaishika sheria yako, Naam, nitaitii kwa moyo wangu wote.
            (K) Uniendeshe katika mapito ya maagizo yako, Ee Bwana.
       (3).    Uniendeshe katika mapito ya maagizo yako, Kwa maana nimependezwa nayo. Nami nitaitii sheria yako daima, Naam, milele na milele.
            (K) Uniendeshe katika mapito ya maagizo yako, Ee Bwana.

     SHANGILIO
1Pet. 1:25
             Aleluya, aleluya, Neno la Bwana hudumu hata milele, na neno hilo ni neno lile jema lililohubiriwa kwenu. Aleluya.

      SOMO LA INJILI
      Lk. 8:19 – 21
              Walimwendea Yesu mama yake na ndugu zake, wasiweze kumkaribia kwa sababu ya mkutano. Akaletewa habari akiambiwa, Mama yako na ndugu zako wamesimama nje wakitaka kuonana nawe. Akawajibu akasema, Mama yangu na ndugu zangu ndio hao walisikiao neno la Mungu na kulifanya.

Copy right© by shajara and published by  MAMBO YAHUSUYO IMANI BLOG
website:

NYIMBO ZA DOMINIKA YA 29 YA MWAKA- C WA KANISA.

Nyimbo za Jumapili ya 29 Mwaka C Karibu kwa ajili ya nyimbo za Jumapili ya 29 Mwaka "C" Mwanzo: Ee Bwana Nimekuita  ...